WASANII
nyota wa Tanzania wanaounda kundi la Kigoma All Stars, wakiongozwa na
Diamond Platinum watakuwepo Mombasa, Kenya wakati wa Robo Fainali za
Kombe la Mataifa ya Afrika Mashariki, CECAFA Challenge.
Tanzania Bara, Kilimanjaro Stars inamenyana na Uganda, The Cranes kesho Uwanja wa Manispaa, Mombasa, Kenya katika Robo Fainali na ujio wa wasanii hao unatarajiwa kuongeza hamasa kwa wachezaji kufanya vizuri.
Mbali na Diamond, wasanii wengine wanokuja Mombasa ni Ommy Dimples, Abdi Kiba, Chegge, Linex, Recho, Mwasiti, Peter Msechu, Macomando, Maunda Zoro, Queen Darleen na Baba Levo.
Wasanii hao wamealikwa Mombasa kufanya onyesho moja kubwa katika ukumbi wa Big Tree Beach Resort, linaloandaliwa kwa pamoja na Blue Moon kwa kushirikiana na Radio Maisha Jumapili. Wanatarajiwa kuwa Mombasa kuanzia leo na kesho watapata fursa ya kuungana na Watanzania wenzao kuishangilia Kilimanjaro Stars Uwanja wa Manispaa, kabla ya shoo yao Jumapili.
Robo Fainali nyingine ni Kenya na Rwanda kesho pia wakati Jumapili, Zambia itamenyana na Burundi na Ethiopia na Sudan.
Mechi zote za Robo Fainali zitachezwa Uwanja wa Manispaa mjini Mombasa Jumamosi na Jumapili, wakati Nusu Fainali zitarudi Nyayo, ingawa iwapo uwekaji nyasi bandia katika Uwanja wa Moi, Kisumu utawahi kukamilika basi Nne Bora zitachezwa na huko, wakati fainali ni Nairobi.
ROBO FAINALI ZA CHALLENGE… Desemba 7, 2013; Uganda VS Tanzania (Saa 8:00 Mchana) Kenya VS Rwanda (Saa 10:00 Jioni) Desemba 8, 2013 Zambia VS Burundi (Saa 8:00 Mchana) Ethiopia VS Sudan (Saa 10:00 Jioni)
No comments:
Post a Comment