Saturday, May 23, 2015

NDEMLA, ISIHAKA HASSANI WAONGEZA MKATABA SIMBA






BEKI aliyewahi kuripotiwa kutakiwa na Real Madrid Castilla, inayoshiriki Ligi Daraja la Kwanza Hispania, maarufu kama Segunda B, Hassan Isihaka (pichani kulia) amesaini Mkataba mpya wa miaka mitatu na Simba SC.
Mapema mwaka huu, maskauti wa Real Madrid waliozuru Tanzania, walivutiwa na wachezaji wawili wa SImba SC, beki Isihaka Hassan na kiungo Ramadhani Singano ‘Messi’.

Timu hiyo ya pili ya mabingwa wa Ulaya, Real Madrid inayocheza mechi zake Uwanja wa Alfredo di Stefano, kupitia mwakilishi wake, Rayco Garcia iliwasilisha rasmi maombi yake kwa klabu ya Simba SC juu ya wachezaji hao.

Garcia alisema anawataka wawili hao Juni mwaka huu waende Hispania kufanyiwa majaribio katika timu hiyo na kama wakifuzu wataanza maisha mapya Ulaya.

Wakati bado Juni inabisha hodi, Isihaka anarefusha muda wa kuendelea kuitumikia Simba SC hadi mwaka 2018.

Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba SC, Zacharia Hans Poppe amesema  jana kwamba, mbali na Isihaka, kiungo chipukizi Said Hamisi Ndemla naye ameongeza Mkataba wa miaka mitatu pia.
“Chipukizi hawa wawili, wote wataendelea kufanya kazi Simba SC hadi mwaka 2018, na bado tunapitia ripoti ya benchi la Ufundi, ili kuboresha mikataba ya wachezaji wengine ambao tunahitaji kuendelea nao,”amesema Kapteni huyo wa zamani wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ).

No comments:

Post a Comment