Saturday, June 6, 2015

DE GEA AWAAGHA WENZAKE MAN UNITED

KWAHERI: David De Gea awaaga wenzake Old Trafford


MIKONO ya kipa, David de Gea, iliyotumika kuibeba Man United katika msimu uliomalizika hivi karibuni, inadaiwa kuwa imetumika pia kuwaaga wachezaji wenzake kikosini humo hivi karibuni katika uwanja wa mazoezi wa timu hiyo, Carrington.
Inadaiwa kipa huyo hataivaa tena jezi ya Man United na ripoti za England zinadai ameshawaaga wachezaji wenzake, benchi la ufundi na wafanyakazi wa klabu.
Staa huyo aliyenunuliwa kwa Pauni 18 milioni Juni 2011 na kuwa kipa ghali England, amegoma kusaini mkataba mpya Old Trafford ambao ungemfanya awe analipwa Pauni 200,000 kwa wiki.
Rais wa Real Madrid, Florentino Perez anaamini atampata De Gea kwa Pauni 25 milioni tu kwa kuwa mkataba wake Old Trafford umebakiza miezi 14 na kipa huyo mzaliwa wa Madrid, amedhamiria kurudi katika jiji hilo ambalo ni makazi ya mpenzi wake, Edurne Garcia Almagro, staa wa muziki wa Pop.
Madrid ilikuwa inasubiri imalize suala lake la kuachana na kocha, Carlo Ancelotti, kabla ya kumgeukia De Gea ambaye atakuwa mbadala wa muda mrefu wa kipa wao, Iker Casillas, ambaye nyakati zinaonekana kumpita.
Kocha wa Man United, Louis van Gaal, ambaye yupo likizoni Ureno, amekiri hana ubavu wa kumzuia kipa huyo asiondoke kurudi kwao Hispania.
“Sidhani kama ninaweza kumshawishi abaki kwani anajua kila kitu ilichonacho Man United. Sihitaji kusema lolote, yeye mwenyewe anahisi kila kitu. Umewaona mashabiki (wanavyompenda) inashangaza sana. Atakapoondoka, atapoteza hilo. Ana sifa nyingi. Inabidi aamue mwenyewe,” alisema Van Gaal.
Licha ya kubembelezwa kiaina na Van Gaal, De Gea ametoa kauli inayoashiria kwamba ataondoka baada ya kutotaka kuzungumzia hali yake ya baadaye huku akisisitiza yuko likizo kwa sasa.

No comments:

Post a Comment